Monday, April 11, 2011

Freeman Mbowe atoa Tamko.....


SIKU moja baada ya Kamati Kuu ya CCM (CC) na Sekretarieti yake kujiuzulu, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amewataka wajumbe wote waliojiuzulu ambao wana nyadhifa serikalini kuondoka madarakani pia.
Mbowe alisema hayo jana katika kongamano la wasomi wa vyuo vikuu lililoandaliwa na chama hicho Mjini Dodoma.
Alisema utamaduni wa kujiuzulu kwa viongozi wa CCM kwa kupisha wenye uwezo kufanya kazi, ungekuwa na maana zaidi kama ungefika katika nafasi za Serikali ambako nako alisema kuwa kunatakiwa kuvuliwa gamba.
Kiongozi huyo wa Kambi ya Upinzani Bungeni alisema kama ilivyo kwa kila mtu muungwana kueleza ukweli pale anapoona kuwa kazi imemshinda, ndivyo inavyotakiwa hata kwa Serikali kwani kwa mujibu wa maelezo yake kuna watu wengi ambao hawajui wajibu wao na kwamba wamekuwa wakifanya kazi kwa mazoea kwa ajili ya kuwafurahisha wakubwa wao.
“Tunawashukuru CCM kwa kuelewa kuwa kutokuwajibika dawa yake ni kujiuzulu, tunataka utamaduni huu waupeleke serikalini na siyo ndani ya chama kwani hilo halitasaidia kitu," alisema Mbowe na kuongeza;
“Tunawaona wanajiuzulu ndani ya chama lakini hawajiuzulu serikalini na serikalini ndiko wanakowakosea wananchi siyo kwenye chama kwa nini wanakataa kujiuzulu serikalini?"
Mwenyekiti huyo alisema kuwa kitendo cha Kamati Kuu ya CCM (CC) na sekretarieti yake kujiuzulu ni ishara ya kuweweseka na kukiri udhaifu akisema sasa yamewafika (CCM) shingoni ndipo wanaweka mambo hadharani.
“Kama Kamati Kuu na sekretarieti vimeonekana ni legelege na dhaifu ni wazi kuwa hata fikra zinazoongoza taifa nazo ni dhaifu na legelege,” alisema.
Alisema kama wanaCCM watavuana madaraka haitasaidia kitu kwa kuwa watu bado ni walewale wasiowajibika katika ngazi zote na siyo kwa kamati kuu peke yake.Kwa mujibu wa Mbowe, tatizo la CCM halipo kwenye gamba, bali ndani ya damu hata kama wakijivua gamba bado damu yao imejaa 'saratani,' akahoji kujivua gamba kama ndiyo suluhisho la matatizo.Alisema hatua ya kamati kuu na sekretarieti ya CCM ya kujiuzulu imewapa wao ari na nguvu zaidi wa kujiimarisha.

Chadema na vyombo vyake vya habari
Akizungumza na wasomi katika kongamano hilo, Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika alisema kutokana na changamoto kubwa wanayoiona hivi sasa ndani ya CCM ni wazi kuwa kunahitajika maandalizi ya kutosha na kwamba wana uhakika kuwa wataibuka washindi 2015.
Mnyika alisema baada ya kuona CCM wanataka kuamka, Chadema kinapanga kuanzisha vyombo vya habari kwa ajili ya kuwapasha habari wananchi."Pamoja na mambo mengine, Baraza Kuu litapitisha mpango kabambe wa miaka mitano katika kuanzisha vyombo vya habari. Tunaamini kuwa wananchi wengi wanakosa kusikia mambo mazuri yanayozungumzwa na viongozi wao.

No comments:

Post a Comment